Maoni of Thursday, 14 November 2019
Columnist: mwananchi.co.tz
Ni kwa kiasi gani fimbo au viboko vinawasaidia watoto katika muktadha mbalimbali wa maisha? Jambo hili linahitaji mjadala na mabishano ya muda mrefu na bado wahusika wanaweza wasifikie muafaka kirahisi.
Mijadala ya fimbo ni migumu kutokana na falsafa, maono na fikra kinzani zinazoendana na utashi wa watu wanaolitizama jambo lenyewe, utata uliomo katika jambo lenyewe na utamaduni wa jamii husika.
Mtizamo wa kifamilia
Kila familia ina malezi yake ambayo huamua aina ya adhabu ambayo watoto hukutana nayo pindi wanapotenda makosa. Adhabu hizo hutofautiana kutokana na ukubwa wa makosa ambayo mtoto anakuwa ametenda. Mathalani, familia yangu kwa maana ya watoto wangu, kwa kawaida hawachapwi fimbo kwa makosa yote madogomadogo au ya bahati mbaya, ya kila aina, lakini huchapwa pale wanapofanya makosa makubwa mara ya kwanza au makosa ya kati yanayojirudiarudia.
Ukubwa au udogo wa kosa au kipimo cha kosa pia ni mjadala unaootegemea falsafa nyingi zisizo na majibu. Kwa kifupi kila familia ina namna ya malezi ambayo yanapima uzito na ukubwa wa kosa alilotenda mtoto na aina ya adhabu itakayofuatia.
Ziko familia ambazo mtoto akifanya kosa dogo sana anachapwa, akifanya kosa la kati anachapwa pia, akifanya kosa la juu anachapwa vilevile.
Ziko familia ambazo hata mtoto akifanya makosa makubwa haguswi, makosa makubwa kwa mtizamo wa kifamilia ambao nimeutumia kulea watoto wangu ni ile hali ya makosa ambayo yana madhara makubwa katika tabia za mtoto atakapokua mkubwa. Mathalani, ikiwa mtoto anagoma kutenda jambo aliloelekezwa kutenda, nyumbani kwangu hilo ni kosa kubwa na linastahili fimbo kwa mtoto mpaka siku atakapoacha.
Kwamba mtoto anaweza kuropoka neno fulani baya kwa mara ya kwanza akaonywa na kufahamishwa, lakini mtoto yuleyule akitumwa dukani akakataa kwenda, hilo si kosa la mazungumzo peke yake, kwa hakika ni mazungumzo na viboko.
Lakini ziko familia ambazo, hata mtoto akigoma kutenda maelekezo aliyopewa, hawezi kuguswa na huendelea kulindwa na kutetewa. Hizi ni aina ya familia ambazo wazazi wamewaacha watoto wajiamulie masuala wenyewe, wazazi wakiamini kuwa namna bora ya kulea watoto ni kuwapa uhuru wa kuamua hata wanapotumwa majukumu na wakubwa.